October 6, 2012

KUCHIMBA MADINI KAZI! NGARA MADINI YAPO KUMBE!



                Unaambiwa Mwanaume kazi!Hii ni Ngara

Na Shaaban ndyamukama-ngarakwetublogspot.com

Mchimbaji Elias Zacharia akitoka shimon

Mchimbaji anayefahamika kwajina la Nzigiyimana akiwa nje ya Shimo la futi 60




Vijana wawili wanaokadiriwa kuwa na umri wa miaka 35 na 40 wanaishi katika mazingira hatarishi katika pori la Nyanzari na Nyakafandi wilaya ya Ngara mkoani Kagera  wakitafuta maisha kwa kuchimba na kupasua miamba kwa mkono  ili kuweza kupata madini ya dhahabu wakitumia mikono kuchimba kupasua miamba
    Wakiongea na  mwandishi wa habari hizi katika pori la maeneo hayo vijana hao wamesema wanatafuta madini aina ya Dhahabu na uchimbaji wake ni mugumu kutokana na shimo kuwa na mwamba unaosababisha kushindwa kufikia dhahabu umbali wa futi 70 kupata madini hayo
Mmoja wa vijana hao Nizigimana Samsoni mkazi wa wilayani Geita amesema kuwa wako katika kata zaRulenge na  Muganza wilayani Ngara  wakichimba na kupasua miamba  kutafuta dhahabu ambapo shimo wanalolichimba limefikia urefu wa futi 60 tangu mwezi februari mwaka huu hadi sasa

Samsoni alisema katika kujitafutia ajira wanachimba na kupasua mawe kwenye miamba na tayari wamepata madini ya Nickel na mawe aina ya Qwagis na wataalamu wao wa madini walioko mkoani Geita wamefanya uchunguzi na kubaini kuwa dhahabu inaweza kupatikana kati ya futi 66  hadi 70.
Alisema mawe meupe yanayofanana na glasi wameagiza wateja wa kununua mawe hayo kwani wapimapo mchanga kwa vipimo vya  asili kwa kutumia karai na maji wameshagundua cheche za kuwepo dhahabu na kuleta matumaini ya kupata madini hayo.Aliongeza kuwa  katika kujitafutia ajira ya kuchimba shimo hilo na kupasua mwamba tangu waanze mwezi februari mwaka huu  viongozi wa kijiji cha Rulenge na Mukubu nawale wa kata ya Muganza  kata wamekuwa wakiwakamata vijana hao kwa madai ya kuharibu mazingira na kuwakatisha tamaa vijana wengine wanaohitaji kujiajiri kwa kutumia nguvu zao

Alidai kuwa wanatumia nyenzo duni   za kufanyia kazi na shughuli yao kuwa  ngumu kwani wanatumia magunia ya kubebea mawe na udongo wakifunga kamba kuvuta udongo au vipande vya mawe kutoka shimoni  na kuchelewa kutimiza malengo yao ya kupata dhahabu mapema .“Zana tunazotumia  kutafuta madini ya dhahabu ni nyundo na tindo kupasua mawe katika miamba na huvuta kamba iliyofunga gunia la udongo au vipande vya mawe toka shimoni kwa kuzungusha gogo lililo katika miti miwili ya matawi kama mashine kurahisisha uvutaji wa mzigo kwa urahisi”.Alisema
    Kwa upande wake Elias Zacharia amesema kuwa changamoto nyingine ni ukosefu wa kituo cha kupata matibabu mara wapatapo msukosuko wa kiafya na hulazimika kutembea umbali mrefu kwenda kutafuta matibabu Mukubu ,Munjebwe au Bukiriro ambapo ni mbali na makazi yao
Alisema kuwa mara washindwapo kufika kwenye vituo vya huduma za afya hulazimika kuwatafuta watu wa kwenda kuwanunulia dawa katika maduka ya dawa baridi katika mji mdogo wa  Rulenge ili kuzuia kwa muda vinyemelezi vya magonjwa pasipo kupima au kupata ushauri wa maafisa tiba za binadamu
Hata hivyo viongozi wa vitongoji vijiji na kata walipohojiwa kuhusu vijana hao walidai madini yanayopatikana eneo hilo ni aina ya Nickel ambapo makampuni kadhaa yamefika na kupima na upatikanaji wake ni kutumia mashine sio mikono. Afisa mtendaji wa kata ya Rulenge Richard Sentoz  na Diwani wa hiyo Hamis Baliyanga walisema kuwa vijana hao wakishindwa kupata wanachotafuta watarudi katika familia zao  kuendelea na shughuli za maisha yao kama kawaida ili mradi walinde mazingira wanayotumia.

Eneo la Nyakafandi ,Nyanzari na maeneo mengine katika kata za Rulenge Muganza Bugarama  pamoja Bukiriro yanafanyiwa utafiti mara kwa mara na kampuni ya Kabanga Nickel tangu mwaka 2005 kuwa na madini ya dhahabu ,Nickel ,a madini mengineyo ambapo serikali inatarajia kufungua mgodi wa Nickel utakao dumu miaka 25 hadi 30 (under ground )na mchakato wa kuhamisha walio ndani ya mradi umeanza ili wahusika waweze kulipwa fidia ya mali walizo nazo katika eneo la mradi.

                            Habari imeandikwa na Shaaban Ndyamukama

No comments:

Post a Comment