July 13, 2014

BUSARA YA UKAWA INAHITAJIKA-KATIBA BORA

Sauti za viongozi wa kisiasa, kiserikali na madhehebu ya dini kuwaasa na kuwasihi Ukawa warejee bungeni zimesikika, kazi sasa ni kwa wajumbe wa kundi hilo kuitikia wito huo au kuziba masikio.
Matamshi ya viongozi hao kwa nyakati tofauti, yameeleza wazi na kuwataka wabunge hao kutengua misimamo yao na kurejea bungeni ili kuchuana, kushindana kwa hoja na kukosoana wakiwa ndani ya Bunge, si nje ya chombo hicho cha kikatiba na kisheria au kufanya mikutano ya hadhara nchi nzima.
Viongozi hao kwa nyakati tofauti, wameeleza kuwa itakuwa busara ikiwa upande wa wabunge waliobaki ndani ya Bunge na wale waliotoka nje, wakakaa pamoja kwa kuzitumia kamati ya mashauriano, iliyopo.
Miongoni mwa viongozi waliotoa wito wa kuwataka Ukawa warejee bungeni ni Rais Jakaya Kikwete, Makamu wa Rais Dk Mohamed Gharib Bilal, Waziri Mkuu Mizengo Pinda, Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar Balozi Seif Ali Idd na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Dk Hussein Mwinyi.
Wengine ni Msajili wa Vyama vya Siasa Jaji Francis Mutungi, Askofu wa Kanisa la Katoliki Jimbo Iringa Tarcius Ngalalekumwa na Mufti Mkuu wa Bakwata Sheikh Shaaban Bin Simba.
Hata hivyo Ukawa wameeleza kuwa wamelisusa Bunge la Katiba, baada ya kujitokeza matusi, kejeli na maneno ya ubaguzi kutoka kwa wajumbe wa CCM, ambao wanadaiwa kuwa waliacha kujadili hoja za msingi na kuanza malumbano kinyume na dhamira ya kuundwa Bunge maalumu la Katiba.
Pia wanaeleza na kutoa masharti kuwa Rasimu ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba, ijadiliwe kama ilivyo, isipunguzwe kipengele wala kifungu chochote na kwamba ushauri au maoni ya Tume yabaki vilevile kama yalivyo bila ya kutiwa mikono au kuchakachuliwa.
Madai haya ya Ukawa kwa upande mmoja yanaleta mkanganyiko na kutia hofu. Kazi ya Bunge maalumu la Katiba ni kuipitia rasimu, kuijadili, kuongeza au kupunguza yaliyomo kwa masilahi ya taifa pale inapobidi, si kuwa muhuri wa kuidhinisha matakwa ya tume yatokanayo na makamishna wao kwa kulitumia Bunge, kabla ya kuitishwa kura ya maoni.
Pia Ukawa wanamtupia lawama Rais Kikwete na kumtaja kuwa ndiye chimbuko la kuvurugika kwa mchakato huo, baada ya kutoa maoni yake kama Mkuu wa Nchi.
Dai hili kwa maoni yangu naona kama limekosa nguvu ya hoja kutokana na Rais kuwa na haki ya kutoa maoni kama ambavyo makamishna wa Tume na Mwenyekiti wao walivyotoa.
Rais pia ana haki ya kutoa maoni yake kwa niaba ya chombo anachokiongoza ambacho ni serikali na kwa niaba ya taifa akiwa Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama.
Anapotakiwa anyamaze, afumbe mdomo au aache mambo yaende kama yanavyotakiwa na wengine, hapo atakuwa anapoteza sifa ya kuitwa Rais wa Nchi na kiongozi wa Serikali.    Source:Mwananchi

No comments:

Post a Comment