July 5, 2014

Warioba ataja sifa za rais 2015


Dar es Salaam. Waziri Mkuu mstaafu, Jaji Joseph Warioba ametoa dira ya urais katika Uchaguzi Mkuu ujao kwa kutaja sifa za rais anayefaa kuiongoza Tanzania.
Warioba alisema kwamba taifa la Tanzania linastahili kuongozwa na vijana wenye nguvu ya mwili na akili. “Mimi nafikiri tuangalie kati ya vijana tulionao, nani anatufaa kuiongoza nchi, tusirudi kuangalia wazee,” alisema Jaji Warioba.
Alitoa kauli hiyo alipokuwa akijibu maswali ya mwandishi wa habari hizi katika mahojiano maalumu yaliyofanyika wiki hii ofisini kwake jijini Dar es Salaam.
Kauli hiyo ya Jaji Warioba imekuja huku ukiwa umesalia takribani mwaka mmoja na miezi minne, kabla ya taifa kuingia kwenye kinyang’anyiro cha Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani utakaoshirikisha vyama zaidi ya 23 vyenye usajili wa kudumu nchini.
Uchaguzi huo mkuu ambao ni wa tano wa vyama vingi nchini, unatarajiwa kulipatia taifa rais mpya, baada ya Rais Jakaya Kikwete kumaliza muda wake wa utawala wa awamu ya nne.
Mbali na wagombea wa vyama vya upinzani, ndani ya CCM pekee kunatajwa kuwa na makundi zaidi ya manne yanayotarajia kuwania urais mwaka ujao.
Makundi hayo ni pamoja na linalotajwa kumuunga mkono Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa, kundi lingine linatajwa kuwa nyuma ya Samuel Sitta ambaye sasa ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki pamoja na linalomuunga mkono Bernard Membe, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa. Pia Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Sera na Uratibu, Stephen Wassira anatajwa kuwania nafasi hiyo ya juu ya uongozi nchini.
Hata hivyo, viongozi hao wamekuwapo madarakani katika nyadhifa na nyakati tofauti huku pia wakiwa na umri uliovuka ujana, unaopendekezwa na Jaji Warioba.
Ndani ya CCM vijana wanaotajwa kutaka kuwania urais mwakani ni pamoja na Waziri wa zamani wa Nishati na Madini, William Ngeleja na Naibu Waziri wa Sayansi na Teknolojia, January Makamba.
Makamba tayari ametangaza nia yake ya kuwania urais akisema huu ni wakati wa kupisha fikra mpya kuongoza dola, licha ya chama hicho kuzuia kutangaza nia na kupiga kampeni kabla ya muda.
Makamba, mmoja wa makada wa CCM walioonywa na chama hicho baada ya kutuhumiwa kuanza kampeni mapema, alijipigia debe kuwa iwapo atapitishwa na chama hicho, ataelekeza nguvu kwenye vipaumbele vinne ambavyo ni ajira, huduma za jamii, uchumi imara na utawala bora. Akizungumzia uzoefu Makamba alisema hakuna ushahidi wowote kwamba miaka mingi kwenye siasa ndiyo inatengeneza kiongozi mzuri.


“Uongozi mzuri unatengenezwa na haiba, wajihi, dhamira, uwezo, maadili, uhodari, hekima na maarifa.   Sifa hizi hazipatikani kutokana na uzoefu wa miaka mingi kwenye siasa hata baadhi ya vijana wanazo,” alisema Makamba.
  Source:-http://www.mwananchi.co.tz/

No comments:

Post a Comment