August 8, 2014

KATIBA

Wasomi wataka wanasiasa waondolewe Bunge la Katiba


 SOURCE:-Mwananchi

Dar es Salaam. Wasomi na wataalamu mbalimbali wameshauri kuangaliwa upya kwa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ili kuwabana wajumbe wanaotumia vikao vya Bunge Maalumu kujijenga kisiasa kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu 2015, badala ya masilahi ya wananchi.
Wamesema Bunge hilo linakosa maridhiano kwa kuwa wajumbe wake wanatetea masilahi yao ya kisiasa badala ya maoni ya wananchi ambayo waliyapendekeza wakati Tume ya Mabadiliko ya Katiba ikikusanya maoni.
Agosti 2, mwaka huu wakati wa mdahalo uliohusu mivutano ya makundi katika mchakato wa Katiba Mpya, Mkurugenzi wa Shule ya Sheria ya Kenya (KSL), Profesa Patrick Lumumba alisema katika maeneo mengine, sheria huwabana wajumbe wanaoteuliwa kuingia kwenye Bunge la Katiba kuwania nafasi za kisiasa hadi baada ya miaka mitano, ili kuepuka kupitisha mambo kwa masilahi binafsi.
Akizungumzia hoja hiyo jana, Rais wa zamani wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Felix Kibodya alisema: “Wanasiasa wameuweka rehani mchakato wa kupata Katiba Mpya. Kosa la kwanza tulilofanya ni kuruhusu wabunge wa Jamhuri ya Muungano na Baraza la Wawakilishi kuwa wajumbe wa Bunge hilo.”
Alisema wawakilishi wa taasisi mbalimbali zisizo za kiserikali na kutoka makundi mbalimbali (si ya kisiasa) ndiyo waliotakiwa kuwa wajumbe wa Bunge hilo.
“Mwakani ni uchaguzi na wajumbe wengi wanalenga zaidi jambo hilo. Hata ukitazama mchakato wenyewe, utaona haujahusisha zaidi wanasheria kama ilivyo kwa nchi kama Kenya,” alisema Kibodya.
Mtaalamu wa lugha na falsafa nchini, Faraja Christoms alitaja makosa matatu yaliyofanyika kuwa ni kuruhusu Rais kuteua wajumbe wa Bunge hilo, wanasiasa kuwa sehemu ya wajumbe na kuruhusu mchakato huo kutawaliwa na wanasiasa.
“Nadhani Rais Kikwete angevunja Bunge la Katiba ili fedha za kuwalipa wajumbe wake kwa muda wote watakaokaa Dodoma zipelekwe kuwalipa walimu na watumishi wengine wa Serikali,” alisema.
Alisema sifa za mjumbe wa Bunge hilo kwanza ni kutokuwa mwanasiasa na hata akiwa, sheria ieleze kuwa hataweza kugombea uongozi kati ya miaka mitatu hadi mitano na kwamba mjumbe huyo asiruhusiwe kuwa na ajenda ya chama au kundi alilotoka.
Mwanasiasa mkongwe nchini, Balozi Job Lusinde alisema: “Tatizo lilianza baada ya kuchagua wajumbe wa Bunge la Katiba na kuwachanganya na wajumbe wengine ambao ni wabunge wa Bunge la Jamhuri na Baraza la Wawakilishi.
“Tulitakiwa kuwa na wajumbe wa Bunge la Katiba kutoka makundi mengine, lakini si wanasiasa wala wabunge.”
Balozi Lusinde alisema idadi kubwa ya wajumbe hao wanatetea masilahi yao yanayolenga uchaguzi mkuu ujao na kwamba kwa mtindo huo ni vigumu Katiba Mpya kupatikana kwa sasa.

No comments:

Post a Comment