February 12, 2013

BUSERESERE,Waislamu, Wakristo wamwaga damu

Defender la Polisi likilanda mitaani kuimarisha hali ya usalama na kutuliza fujo

Askari akiendeleza harakati za kuimarisha usalama

Kikosi cha FFU

Hii ndio nyama inayosadikiwa kuwa chanzo cha Vurugu, imechinjwa na wakristu jambo linalipongwa kuwa hawana mamlaka ya kuchinja

Waraka uliohamasisha wakristu kushiriki katika uzinduzi wa siku ya Kuchinja

Majeruhi wa tukio hilo

Kijana aliyejeruhiwa baada ya kupatiwa huduma ya kwanza


Baadhi ya wakazi wa kata za Buseresere na Katoro katika wilaya za Chato na Geita wameilalamikia serikali kushindwa kutoa tamko hali iliyopelkea vurugu na mauaji ya Mchungaji wa kanisa la P.A.G.T na baadhi ya raia kujeruhiwa vibaya

Wananchi hao wamesema hayo ikiwa ni siku moja baada ya mapigano ya waislam na wakristo kutokea katika kata ya buseresere wilayani Chato

Mmoja wa wananchi hao Bw. Paschal Magoho amesema Serikali ilitakiwa kuchukua jitihada za maksudi mapema ili kuzuia vurugu hizo

Katika vurugu hizo,Mali za wananchi zimeharibiwa vibaya huku baadhi ya maduka na bidhaa zikiteketezwa kwa moto
Miongozi mwa wananchi walioharibiwa mali zao ni Pamoja na Mwenyekiti wa Baraza la waislam Tanzania wa wilaya ya Chato  na mwenyekiti wa CCM kata hiyo Bw.Yusuf Idd Banana ambaye ametaja mali zilizoharibiwa kuwa na thamani ya Shilingi milioni 10.

Ugomvi huo uliosababisha mauaji, majeruhi na uharibifu wa mali umetokana na hoja ya wakristu wakitaka kuwa na mamlaka ya kuchinja mifugo na kupinga dhana kuwa wenye mamlaka ya kuchinja ni waislam pekee, na kwamba waislam wanapochinja   wakristu wanakula, jambo ambalo linaelezwa kuwa ni kinyume na wakristu wakichinja waislam hawali!..............................................Eeemungu, tuepushe na dhambi ya UDINI..

Vyombo vingine   vya habari vimeandika:-

VURUGU kubwa za kidini kati ya Waislamu na Wakristo, zimezuka katika kijiji cha Buseresere, wilaya ya Chato, mkoani Geita, na kusababisha kifo cha Mchungaji wa Kanisa la Pentekoste Assemblies of God, Mathayo Kachila (45), huku watu wengine 10 wakijeruhiwa vibaya kwa mapanga.

Mchungaji huyo alichinjwa na watu wanaodaiwa ni kuwa waumini wa Kiislamu kisha mwili wake kutelekezwa kwenye vibanda vya maduka ambavyo viko jirani na eneo hilo jana.

Taarifa kutoka eneo la tukio hilo zilisema kuwa tukio hilo lilitokea asubuhi ambapo chanzo chake kinatajwa kuwa ni watu wanaodaiwa kuwa wafuasi wa Kiislamu kuvamia bucha iliyokuwa ikiwauzia nyama Wakristo wa kijiji hicho waliokuwa wamepanga foleni kwa wingi kusubiri huduma hiyo.

Wakiristo hao walikuwa wamechinja ng’ombe mmoja na mbuzi wawili eneo la kanisani kabla ya kuipeleka nyama hiyo katika bucha hiyo iliyoko eneo la Buseresere Sokoni na ndipo walipokumbana na kadhia.

Mashuhuda walisema kuwa tukio hilo lilianza saa 2:00 asubuhi muda mfupi baada ya nyama kuwasili katika bucha hiyo ya Wakristo kwa ajili ya kuuzwa, jambo linalodaiwa kuwakera Waislamu ambao waliivamia bucha hiyo kwa lengo la kuifunga.

Taarifa ziliongeza kuwa wakati Wakristo wakitafakari uwepo wa Waislamu kwenye bucha yao, ghafla walishtukia wenzao hao waliokuwa wametapakaa kwa wingi wakiimwagia nyama hiyo vitu vinavyodaiwa kuwa sumu.

Kutokana na hali hiyo, Wakiristo walioonekana kukerwa na kitendo hicho na ndipo mapambano yalipoanza kati ya pande hizo mbili huku Wakristo wakitumia mawe na Waislamu wakitumia mapanga na majambia.

Ilidaiwa kuwa wakati mapambano hayo yakiendelea, mchungaji huyo ambaye kwa sasa ni marehemu alifika eneo la tukio ili kujua kulikoni na ndipo alipojikuta akishambuliwa kwa mapanga sehemu mbalimbali za kichwani na kupoteza maisha akikimbizwa katika Hospitali ya Wilaya ya Geita kwa matibabu.

“Yaani ilikuwa kama mzaha tu...baada ya Wakristo kuleta ng’ombe mmoja na mbuzi wawili kwenye bucha yao, tulishangaa kuona Waislamu wamevamia hiyo bucha wakati tayari nyama ikiwa inauzwa na Wakristo wakiwa wamepanga foleni wakisubiri kuhudumiwa,” alisema shuhuda mmoja.

Aliongeza kuwa Waislamu walipofika walitaka kuifunga ile bucha lakini Wakristo waligoma na ndipo wengine walifika na kuimwagia ile nyama vitu kama sumu na huo ukawa mwanzo wa machafuko.

“Kwa vile wenzetu walifika eneo hilo wakiwa na silaha tayari walianza kuwakata Wakristo na kuivunjavunja ile bucha huku Wakristo wakijihami kwa kutumia mawe lakini walizidiwa nguvu,” alisema shuhuda mwingine.

Waliojeruhiwa ni Saidi Ntahompagaze (45), Sadick Yahaya (40),Yasin Rajab (56),Vicent Damon (22), wote wakazi wa Buseresere na mtu mmoja aliyefahamika kwa jina moja la Ramadhan ambaye yuko mahututi katika wodi namba nane katika hospitali ya wilaya ya Geita.

Hata hivyo watu wengine watano ambao majina yao hayakuweza kupatikana mara moja walitibiwa na kuruhusiwa kutokana na hali zao kuwa nzuri.

Polisi kutoka wilaya za Chato na Geita walifika eneo la tukio hilo saa 4:30 na kukuta uharibifu mkubwa umekwishafanyika ikiwa ni pamoja na duka la Mwenyekiti wa BAKWATA Wilaya ya Chato, Yusuph Idd, linalotumika kwa biashara ya M-Pesa na vinywaji baridi likiwa linateketea kwa moto.

Mkuu wa Wilaya ya Chato, Ludorick Mpogolo, aliyefika eneo la tukio muda mfupi baada ya polisi kuwasili, mbali na kusikitishwa na kitendo hicho aliwataka wananchi kuwa watulivu wakati serikali ikiangalia njia sahihi za kutatua mgogoro huo ambao unakua kwa kasi kila kukicha.

Hivi karibuni mgogoro huo wa kidini umezidi kukua wilayani humo kwa pande hizo mbili kila upande ukidai ndiyo wenye haki ya kuchinja nyama inayouzwa buchani

No comments:

Post a Comment