February 24, 2013

Kiongozi wa NCCR MAGEUZI ASIMAMISHWA

Na Mrisho Salum-NGARA
Chama cha NCCR-Mageuzi mkoani Kagera kimemsimamisha mwenyekiti wa chama hicho wilayani Ngara Bw Kennedy Stanford Festo kwa kukiuka katiba ya chama chake na kushiriki maadhimisho ya kuzaliwa kwa CCM

Kamishna wa chama hicho mkoani Kagera Bw Peterson Mushenyera amesema kuwa uamuzi huo umefikiwa katika kikao cha kamati tendaji ya chama hicho wilaya ya Ngara kilichofanyika juzi

Amesema kuwa Bw Festo amesimamishwa kwa muda wa siku 14 kutokana na kuvunja katiba ya chama chake na kuhudhuria maadhimisho ya kuzaliwa kwa CCM yaliyofanyika February 5 katika kata ya Kabanga wilayani Ngara

Bw Mushenyera amesema kuwa Bw Festo pia ameandikiwa barua ya kujieleza kwa kamati ya nidhamu ya chama hicho wilayani Ngara inayoongozwa na mwenyekiti Wyclif Samwel
Amenukuliwa akisema Ninasema tunamsimamisha uenyekiti mpaka kesi yake itakapo kwisha na chama chetu hakina ushirikiano na chama cha mapinduzi

Aidha kamati hiyo ya utendaji ya NCCR-Mageuzi wilayani Ngara imemteua Bw Joseph Bucha kukaimu nafasi ya mwenyekiti wa chama hicho wilayani Ngara katika kipindi alichosimamishwa Bw Festo

No comments:

Post a Comment