Kamanda wa Polisi Mkoa wa Temeke, Engelbert Kiondo akizungumza wa mkutano na waandishi Dar es Salaam |
Dar/Dodoma. Wakati kukiwa na utata wa kifo cha
Meneja wa Biashara ya Petroli wa Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji
(Ewura), imebainika kuwa tofauti ya takwimu kati ya mamlaka hiyo na
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), iliyotolewa kwenye Kamati ya Bunge ya
Bajeti ni Sh25 bilioni.
Meneja huyo, Julius Gashaza alikuwa akihudhuria
kikao kilichokuwa kikijadili tofauti hiyo bungeni Dodoma na baadaye
aliporudi Dar es Salaam akakutwa amejinyonga hotelini huku ikielezwa
kuwa alirudi akiwa amejawa hofu na kukosa amani.
Vyanzo vyetu ndani ya kamati hiyo vimeeleza kuwa
tofauti iliyobainika katika hesabu za taasisi hizo za Serikali ni lita
11,755,161, ambazo zingeuzwa kwa bei ya sasa ya petroli mkoani Dar es
Salaam ya Sh2,200 zingepatikana Sh25.86 bilioni.
Kwa mujibu wa vyanzo hivyo, takwimu za TRA
zinaonyesha kuwa kati ya Julai 2013 hadi Machi mwaka huu, kiasi cha
mafuta kilichoingizwa nchini kilikuwa lita 2,189,240,000 wakati Ewura
ilionyesha ni lita 2,177,484,839.
Hata hivyo, baada ya utata huo na Kamati ya Bajeti
chini ya Andrew Chenge kuitaka Serikali itoe ufafanuzi wa tofauti hizo,
Serikali iliwasilisha taarifa yake Jumapili ikisema takwimu zote ni
sawa.
Katika ufafanuzi wake, Naibu Waziri wa Fedha,
Mwigulu Nchemba alisema uhakiki wa takwimu hizo ulibaini kuwa zote
zilikuwa ‘sahihi’ na kwamba tofauti iliyopo inatokana na upimaji wa
mafuta.
Nchemba alikaririwa akisema TRA hupima mafuta
kwenye meli mara inapoingia na kukadiria kodi wakati Ewura hupima mafuta
yanapopokewa kwenye matanki.
“Kwa kuwa wakati mwingine meli hutumia muda mrefu
tangu zinapoingia hadi zinapoteremsha mafuta, sehemu ya mafuta ambayo
TRA huhesabu kama yameingizwa katika mwezi mmoja wakati Ewura hupata
takwimu za kiasi cha baadhi ya mafuta hayo katika mwezi unaofuata na
hiyo ndiyo iliyosababisha kuwapo kwa tofauti hiyo ambayo hata hivyo ni
ndogo.”
Kulingana na takwimu hizo, kiasi cha mafuta
kilichoonyeshwa na TRA kilikuwa juu kuliko kile kilichoonyeshwa na Ewura
na haijajulikana iwapo kutofautiana huko kwa takwimu kuliifanya
Serikali kumweka kitimoto Gashaza.
Alikuwa na hofu
Sintofahamu imeendelea kugubika kifo cha Gashaza
na sasa imeelezwa kuwa alirudi kutoka Dodoma akiwa amejawa hofu na
kukosa amani.
Mkurugenzi Mkuu wa Ewura, Felix Ngamlagosi alisema
jana kuwa ingawa hakuzungumza na Gashaza baada ya kurudi kutoka Dodoma,
taarifa za polisi na kutoka kwa mkewe zinaeleza kuwa alirudi akiwa na
hofu na ndiyo sababu ya kuondoka nyumbani kwake na kwenda kulala
hotelini.
SOURCE:-Mwananchi
SOURCE:-Mwananchi
No comments:
Post a Comment