October 29, 2015

John Magufuli ni rais mpya wa Tanzania

Waziri wa ujenzi wa Tanzania John Pombe Magufuli ameshinda kinyang'anyiro cha urais kwa 58% ya kura huku Edward Lowassa, mpimzani wake wa karibu, akipata 39%.

 .........................................................................................................................................................
Jina la Dk. John Pombe Magufuli, au JPM kama linavyofupishwa, halikuwa hata miongoni mwa majina matano yaliyopewa nafasi ya usoni kuteuliwa na chama cha mapinduzi kupeperusha bendera yake katika uchaguzi wa Oktoba.
Lakini wapo ndani ya chama hicho waliyomuona kama karata ya kati, katika wakati ambapo chama hicho kinatafuta kujisafisha kutoka na mkururu wa kashfa za rushwa na kile kinachoelezwa kuwa kasi ndogo ya kuleta maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
Safari yake ya kisiasa
Magufuli mwenye umri wa miaka 55, mwalimu wa hesabati na kemia aliegeuka mwanasiasa amekuwa mwanachama mtiifu kwa CCM tangu mwaka 1977. Alichaguliwa kwa mara ya kwanza kuingia bungeni mwaka 1995 kuliwakilisha jimbo Biharamulo Mashariki -sasa Chato - na baada ya kuchaguliwa kwake aliteuliwa na rais Benjamin Mkapa kuwa naibu waziri wa ujenzi, nafasi aliyoishikilia hadi mwaka 2000, alipopandishwa na kuwa waziri kamili wa wizara hiyo.


Mwaka 2005, rais Jakaya Kikwete alimteuwa kuwa waziri wa Ardhi, Nyumba na maendeleo ya Makaazi, aliyoitumikia kwa miaka mitatu kabla ya kuhamishiwa kwenye wizara ya maendeleo ya mifugo na uvuvi kati y amwaka 2008 na 2010. Baada ya uchaguzi wa mwaka 2010, alirejeshwa kwenye wizara ya ujenzi anayoiongoza hadi sasa.
Marafiki na hata maadui zake hawasiti kuelezea kuridhishwa kwao na utendaji wa Magufuli katika nafasi zote alizozishikilia serikali, mara kadhaa wakimtaja kwa jina la "jembe" ikimaanisha mchapakazi - na hata kwenye kampeni zake, kaulimbiu yake ya "hapa Kazi tu" inaakisi utayarifu wake wa kuendeleza uchapaji kazi.
"Siyo jambo la aibu kutambua jambo jema la kimaendeleo linapofanywa, bila kujali limefanywa na mtu kutoka chama gani cha siasa," alisema mwenyekiti wa taifa wa chama cha Demokrasia na MaendeleoFreeman Mbowe, akisifu utendaji kazi wa Magufuli, wakati wa uzinduzi wa barabara iliyotengenezwa katika jimbo lake la Hai, mkoani Kilimanjaro.
Mtendaji kuliko mwanasiasa
Dk. Magufuli ni mtendaji asiyeruhusu uzembe na anapotaka jambo litendeke, analisimamia na kuhakikisha matokeo yanaonekana. Anakumbukwa kwa hatua yake ya kuikataa barabara mpya iliyojengwa kwa ufadhili wa serikali ya Japan, baada ya kubaini kuwa haikuwa kwenye kiwango kinachotakiwa, na hakuna alielalamika miongoni mwa wananchi na hata serikali.
Hakusita hata kuamuru majengo ya serikali kuvunjwa, pale ilipobainika kuwa yamekiuka sheria za ujenzi, kama vile kujengwa katika maeneo ya hifadhi za barabara.
Baadhi hata hivyo wanahofu kuwa kwa mwendo huu alio nao, huenda akaliongoza taifa kibabe, lakini wafuasi wake wanasema Tanzania kwa hali iliyo nayo inahitaji si tu kiongozi Jasiri , lakini pia mwenye kasi ya utendaji atakaesaidia kuiondolea nchi matatizo yanayoikabili yakiwemo rushwa iliyoota mizizi, na kuchochea kasi ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii.
Mabango ya kampeni ya Dk. John Magufuli. Mabango ya kampeni ya Dk. John Magufuli.
Wakati wa kampeni zake, Magufuli amekiri kuwa yeye ni mkali, na hasa linapokuja suala la kuwaletea wananchi maendeleo, ambayo amekuwa akisisitza kuwa hayana itikadi za vyama. "Nitakuwa dikteta wa maendeleo," aliwahi kusema katika moja ya mikutano yake ya kampeni.
Duru ndani ya CCM zinasema uamuzi wake wa kuchukuwa fomu za uteuzi ulishawishiwa na rais wa awamu ya tatu, Benjamin Mkapa, rafiki yake wa karibu ambaye hakusita hata siku moja kumuunga mkono na kumtetea wakati alipojikuta kwenye matatizo. Hata rais wa awamu ya pili mzee Ali Hassan Mwinyi alimsifu magufuli akimtaja kuwa yeye ni simba wa kazi.
Dk. Magufuli ni mtu wa takwimu, ana kumbukumbu imara na linapokuja suala la kutoa tarakimu, hapati shida kutaja kwa tarakimu pale anapouliwa na ama waandishi wa habari kwenye korido za wizara yake au kwenye shughuli za uzinduzi wa miradi ya ujenzi wa barabara.
Wakati wa mkutano mkuu wa chama mwaka 2010, Magufuli yalitakiwa na mwenyekiti rais Jakaya Kikwete aeleze utendaji wa chama na serikali yake katika sekta ya ujenzi wa barabara, na alijibu kwa kutaja makhsusi idadi ya zinazojengwa na zilizokamilika tayari. Na hakuishia hapo, alitaja pia maeneo - yaani mikoa, wilaya na hata vijiji zinakojengwa.
Kampeni ya mabadiliko
Kama ilivyo na muungano wa vyama vya upinzani, Magufuli anaendesha kampeni ya mabadiliko, akiahidi kushughulikia tatizo la rushwa kwa kuanzisha mahakama ya kuwashtaki wala rushwa. "Kiama cha mafisadi kimewadia," amekuwa akisema Magufuli kaktika karibu kila mkutano wa kampeni aliyouhutubia.
"Sikuomba nafasi hii kwa majaribio, niliomba kwa ajili y akufanya kazi na kuwatumikia watanzania. Naijua vizuri historia ya nchi hii, najua tulikotoka, tiulipo sasa na tunakoelekea," alisema mgombea huyo, na kusisitiza yeye ndiye mtu sahihi wa kuiongoza Tanzania kuelekea huko.
Mabango yanayowanadi wagombea wakuu wa kiti cha urais nchini Tanzania. Mabango yanayowanadi wagombea wakuu wa kiti cha urais nchini Tanzania.
Pamoja na uchapakazi, amekosolewa kwa uamuzi wake wa kuuza nyumba za serikali kwa wafanyakazi na umma. Baadhi pia wanamkosoa kwa kuchukuwa maamuzi ya haraka ambayo wakati mwingine yameigharimu serikali mamilion ya pesa - wakitolea mfano uamuzi wake wa kuikamata meli iliyodaiwa kufanya uvuvi haramu kwenye bahari ya Tanzania - na kisha mahakama kuamua kuwa meli hiyo ilikuwa inavua kihalali na kuiamuru serikali kuwafidia wamiliki kiasi cha shiligi bilioni 2.8.
Wakati fulani Magufuli pia amepishana kauli na wakubwa zake wa kazi, alipokaidi agizo la waziri mkuu Mizengo Pinda kuhusiana na magari yaliyozidisha uzito kuhuruhiwa kupita kwenye barabara za Tanzania, akisema maagizo hayo ya waziri mkuu hayakuwa yanatekelezeka na hayakuwa pia katika maslahi ya nchi.
Dk. Magufuli amepokea tuzo kadhaa ndani na nje ya Tanzania, na ameandika vitabu na makala za majarida katika maisha yake ya kikazi. Na kwa vile aliwashinda wanawake wawili kwenye kinyanganyiro cha uteuzi, aliamua kuwafidia wanawake kwa kumteuwa mwanama Samia Hassan Suluhu kuwa mgombea mwenza wake - na kuweka uwezekano wa kuwa na mwanamke wa kwanza mwakamu wa rais katika historia ya nchi hiyo.

SOURCE:-DW

No comments:

Post a Comment