October 28, 2014

Kiwanda cha matrekta kujengwa Tanzania

Kiwanda cha matrekta kujengwa Tanzania
Source:www.mwananchi.co.tz
 Warsal, Poland. Kampuni ya Ursus ya Poland imesema ina mkakati wa kujenga kiwanda cha kutengeneza matrekta Tanzania kwa kushirikiana na kampuni ya Suma JKT.
Rais wa Bodi ya Ursus, Karol Zarajczyk alisema hayo jijini Warsaw jana wakati Waziri Mkuu Mizengo Pinda alipokutana na wafanyabiashara wenye nia ya kuwekeza Tanzania.
Zarajczyk alisema wanataka kujenga kiwanda hicho kwa kuwa wametambua Tanzania ina fursa ya kufungua milango ya kibiashara kwa nchi jirani za Afrika Mashariki na Kati.
Alisema lengo jingine la kampuni hiyo inayotengeneza matrekta ni kutoa mafunzo kwa wakulima ya jinsi ya kutunza matrekta hayo, ili waone umuhimu wake katika sekta ya kilimo.
“Barani Afrika tulianza kupeleka matrekta Ethiopia, Ghana na Guinea. Sasa hivi tumeamua kwenda Tanzania na Zambia.
“Nia yetu siyo kujenga tu kiwanda, bali pia kutoa huduma kwa wakulima juu ya uendeshaji na utunzaji wa matrekta hayo,” alisema.
Alisema wako tayari kutoa mafunzo kwa vijana wa Tanzania waliopo vyuoni ili waweze kuunganisha matrekta hayo, kuyafanyia ukarabati na kutengeneza vipuri vyake wakati kunapokuwa na ulazima wa kufanya hivyo.
“Tunapenda kujenga kiwanda mahali ambapo itakuwa rahisi kupata vijana wa kuajiriwa ili iwe rahisi kuwafundisha teknolojia tunayoitumia kutengeneza matrekta,” alisema.
Kwa upande wake, Pinda alisema atawasilisha maelezo hayo kwa waziri anayehusika na sekta hiyo ili mawasiliano rasmi ya kujenga kiwanda hicho yafanyike.

No comments:

Post a Comment